Tuesday, October 16, 2018

NGUVU YA WATU UNAOISHI NAO




Ndugu, karibu tena katika mwendelezo wa makala ambazo zimekuwa zikitolewa katika blogu na app ya timiza ndoto ni tumaini langu unaendelea vizuri na kunufaika na mafunzo haya ambayo kimsingi ukisoma na kuyachukulia hatua ni ngazi pekee ya kukufanya ufikie malengo yako na kutimiza ndoto zako.
Leo naenda kuzungumzia swala la msingi sana ambalo linaweza kukufanya ufikie malengo yako au usifikie malengo yako na kutimiza ndoto zako. NGUVU YA WATU UNAOISHI NAO.
Watu unaoishi nao ni kipimo tosha cha kukutambulisha kama unaweza kufikia ndoto zako au la. Kuna msemo wa waswahili ambao unasema  Ndege wanaofanana huruka pamoja ” kwahiyo kupitia watu unaoishi nao tunapata picha nzima ya maisha yako maana mawazo na mtazamo mzima wa watu mnaoishi nao ni lazima ufanane. Kama umezungukwa na watu ambao ni maskini na wana mawazo ya kimaskini hakuna njia yeyote unayoweza kukwepa umaskini kama utaendelea kuwa nao.

Watu ulioko nao karibu kama ndugu, jamaa, marafiki na hata wafanyakazi wenza wana ushawishi mkubwa sana kwako. Unaweza kuwa na mawazo mazuri sana ya kuondoka kwenye umaskini wako ila unapowapa mawazo yako watu wako wa karibu kama wana mawazo ya kimaskini watakuwa wa kwanza kukukatisha tamaa. Ni rahisi sana kuwasikiliza kwa sababu huenda unawaamini sana na pia upo karibu nao sana hivyo unashindwa kuwapinga. Kwa njia hii unajikuta unaendelea kuwa maskini licha ya jitihada nyingi unazofanya za kujikwamua kwenye umaskini huo.

Jaribu kuchunguza vizuri na kwa makini uangalie mfumo wako wa maisha na vitu unavyofanya havitofautiani sana na vile wanavyofanya watu unaoishi nao kwa muda mwingi. Wote ni kama mna mfumo mmoja wa maisha utakuta wote mmeajiriwa au mnafanya biashara , mkitoka kazini labda jioni mnakutana baa kupumzika, hadithi zenu zinahusisha mambo mengine tofauti tu. Kwa njia hii unajikuta wote mna uchumi unaofanana. Kama watu unaoishi nao muda mwingi hawana ndoto kubwa kwenye maisha yao watakuzuia na wewe kuwa na ndoto kubwa. Kama watu hao hawaoni umuhimu wa kubadili maisha yao, watakuambukiza na wewe tabia hiyo.

Sasa ufanye nini kama umeshagundua kwamba watu unaoishi nao wanakuzuia kufikia malengo na ndoto zako. Naomba fanya mambo matatu yafuatayo;

  1.   Punguza muda unaotumia kukaa na watu hao. Jinsi ambavyo unatumia muda mwingi na watu hao ndivyo unazidi kupokea sumu zao. Hivyo kuwa makini na punguza muda unaotumia kukaa na watu hawa , pia angalia ni mambo gani ambayo unaweza kuwashirikisha . kama watu hawa wamekuwa kikwazo kwako kufikia malengo na ndoto zako kwa kukukatisha tamaa acha kuwashirikisha mawazo yako makubwa. Anza kubadili maisha yako taratibu bila ya kuangalia wao wanafanya au kusema nini.
  2. Anza kutafuta watu ambao wana mawazo makubwa na wenye mafanikio ndo utumie muda mwingi kuwa nao. Kwa kukaa na watu wa aina hii utaanza kuambukizwa tabia zao ambazo zimewafanya wakaendelea. Kwa kusikiliza maongezi yao na kuona mitazamo yao inakuwa rahisi sana kwako kubadili mtazamo wako. Kwa kuwashirikisha watu hawa mipango yako mikubwa watakupa moyo uifanye kwani wengi wao walishapita kwenye hiyo na wanajua inawezekana.
  3. Kuwa na mshauri mzuri. Mara nyingine ni vizuri kuwa na mshauri ambaye mnakuwa mnakutana kila baada ya muda unamweleza umefikia wapi na changamoto unazokutana nazo na mshauri huyo anakuwa anakufuatilia na kukusaidia jinsi ya kukabiliana na changamoto mbalimbali unazokutana nazo. Ni vyema mshauri wako awe ni mtu ambaye ameshafanikiwa kwenye hicho unachotaka kufanya. Isiwe unafanya biashara halafu mshauri wako ni mtu ambaye siye mfanyabiashara. Mtu wa aina hii hana msaada mkubwa kwako kwa sababu hajui nadharia ya kile unachokifanya.


Kwa njia yoyote utakayotumia kujiondoa kwenye umasikini hakikisha umezungukwa na watu ambao wana mawazo kama ya kwako na wanaelekea unakoelekea kwa kukaa na watu ambao hawana mpango na maisha yao watakunyonya nguvu yote na mabadiliko yaliyo ndani yako. Ahsante sana kuwa kuwa nami naomba tukutane tena kwa makala ijayo.UNAFANYA KAZI NA NANI?

0 comments: