Friday, October 19, 2018

UNAMFANYIA KAZI NANI?



Habari tena ndugu, ni tumaini langu tena hujambo na unaendelea vizuri. Karibu kwenye mwendelezo wa makala ambazo nimekuwa nikizitoa katika blogu na app ya Timiza ndoto. Ndugu kabla sijaendelea kufafanua zaidi kuhusu kichwa tajwa hapo juu napenda nikusihi kitu kimoja  “ Ubora wa mwalimu darasani unaonekana zaidi pale wanafunzi wake wanapofaulu kwenye mtihani wala siyo darasani tu namna gani anafundisha”  kwahiyo itakuwa haina maana ya kuendelea kufuatilia blogu na app Timiza ndoto kama utaishia kusoma tu bila kuchukua hatua sitahiki katika maisha yako. Naomba twende wote hatua kwa hatua ahsante.
Mpaka sasa unamfanyia kazi nani? Ni kichwa cha makala chenye swali ambalo linahoji kuhusu kazi yako. Hebu tafakari.
Unafanya kazi kukuza mradi wako au unafanya kazi ya kukuza miradi ya watu wengine? Napenda niseme kitu kimoja cha msingi sana hakika kama unamfanyia mtu mwingine kazi nafasi ya kutimiza wewe ndoto zako ni ndogo sana.  Naamanisha kama mpaka sasa umeajiriwa na huna mawazo ya kutoka kwenye ajira yako kuna uwezekanao mkubwa sana wa kusikia tu neon kutimiza ndoto.
Sisemi kwamba ajira ni mbaya au kwenye ajira huwezi fikia ndoto zako. Hebu tuangalie hali halisi, kama umeajiriwa angalia sehemu yako ya ajira ni watu gani ambao wanalipwa fedha nyingi kiasi cha kuwafanya wapate utajiri? Utakuta ni wachache sana , tena ni wakurugenzi na mameneja wakubwa. Nyie wafanyakazi wengine wa kawaida mishahara haikutani , yaani mshahara wa mwezi huu unaisha kabla ya kupata mshahara wa mwezi unaokuja. Hebu tuangalie nafasi ya wewe kufikia kiwango hicho cha ukurugenzi au umeneja! Ni nafasi ndogo sana kwako wewe kupata cheo hicho kwa sababu kipo kimoja tu na wenye sifa wanaweza kuwa wengi. Ndio maana nasema nafasi ya wewe kufikia malengo yako kwa kumfanyia mtu mwingine kazi yaani kuajiriwa ni ndogo sana.
Kama umeajiriwa hata ukafanya kazi kwa kiwango kikubwa kiasi gani bado mshahara wako utakuwa uleule ama utaongezeka kidogo sana. Wakati mwingine unaweza kupewa pongezi kidogo ambayo hailingani na jitihada zako. Ila kama unafanya kazi yako mwenyewe iwe umejiajiri au biashara jinsi ambavyo utaongeza jitihada ndivyo utavyozidi kuongeza kipato chako. Hakuna wa kukupangia kiwango cha kipato ila wewe mwenyewe.
TUFANYE NINI KUFIKIA MALENGO YETU?
Kama tayari upo kwenye ajira anza kufanya mipango ya kujiajiri ama kufungua biashara baadae. Kama bado hujaingia kwenye ajira weka mipango ya kutoingia kabisa au panga kuingia kwenye ajira na kukaa muda mfupi tu ili kupata uzoefu na mtandao na baadae uondoke ukafanye kazi zako. Usisubiri kukaa  kwenye ajira mpaka utakapostaafishwa utashindwa kutimiza malengo yako na ndoto zako.
Ukikaa sana kwenye ajira unajisahau na unakuwa unawaza matatizo tu unayokutana nayo kwenye ajira yako na jinsi mshahara ulivyo kidogo na matumizi makubwa. Hebu kwa mara moja acha kufikiria matatizo hayo ya ajira na ufikiri ni jinsi gani utaondoka kwenye matatizo hayo. Weka mipango ni lini utaondoka na utakwenda kufanya nini?.
Tunaishi kwenye kipindi ambacho tuna fursa nyingi sana za kutengeneza kipato ukiacha ajira. Angalia ni fursa ipi inayokufaa wewe kisha uanze kujifunza vitu vya msingi kuhusiana na fursa hiyo. Kikubwa tumia ujuzi ulio nao, tumia uwezo mkubwa ulio ndani yako pamoja na vipaji vya kipekee ulivyo navyo na angalia mazingira yanayokuzunguka ili uone ni kitu gani cha tofauti unaweza kufanya.
Kwa kujiajiri au kufanya biashara unatengeneza uhuru zaidi wa kuweza kupata kipato kinacholingana na jitihada zako. Pia unaweza kuwasaidia watu wengi zaidi kwa kutengeneza ajira.
Ni katika mwendelezo wa makala zinazopatikana katika blogi na app ya Timiza ndoto karibu tena kwa makala ijayo UMEJITOA?  

0 comments: